Translate

Saturday, March 2, 2019

Kwa Nini Upendo Hupungua?

Kwa Nini Upendo Hupungua?
“Inaonekana kuwa rahisi sana kumpenda mtu kuliko kudumisha upendo huo.”—  SIXBERTY MANSON 
ONGEZEKO kubwa la ndoa zisizo na upendo yamkini si jambo la kushangaza. Ndoa ni uhusiano tata wa kibinadamu, na wengi huingia katika uhusiano huo bila kujiandaa vya kutosha. “Inatubidi kuwa na uzoefu kiasi fulani kabla ya kupokea leseni ya kuendesha gari,” asema Dakt. Dean S. Edell, “lakini cheti cha ndoa chahitaji tu sahihi.”
Kwa sababu hiyo, ingawa ndoa nyingi hunawiri na kuwa na furaha tele, ndoa kadhaa hunyong’onyea katika matatizo. Huenda mwenzi mmoja au wote wawili waliingia katika ndoa wakiwa na matumaini makubwa lakini hawana ujuzi unaohitajika ili kudumisha ndoa. “Watu wanapopendana mara ya kwanza,” aeleza Dakt. Harry Reis, “kila mmoja huwa na uhakika mno na mwenziwe.” Wao huhisi kana kwamba mwenzi wao ndiye “mtu pekee duniani mwenye maoni sawa na yao. Nyakati nyingine hisia hiyo hufifia na inapokuwa hivyo, ndoa huathiriwa sana.”
Jambo la kupendeza ni kwamba ndoa nyingi hazifikii hatua hiyo. Lakini acheni tuchanganue kwa ufupi sababu kadhaa zinazosababisha upendo kufifia katika baadhi ya ndoa.
Kutamaushwa—“Sikutarajia Hali Hii”
“Nilipoolewa na Jim,” asema Rose, “nilitarajia tungekuwa na mapenzi kama ya malkia na mfalme mwenye kuvutia katika hadithi moja—mahaba kemkemu, wororo tele na kutendeana kwa fadhili.” Lakini, baada ya kitambo kidogo, “mfalme” wa Rose akawa havutii tena. “Hatimaye alinitamausha sana,” yeye asema.
Sinema, vitabu, na nyimbo zinazopendwa na wengi hutoa maoni yasiyo halisi kuhusu upendo. Wanapokuwa wakichumbiana, huenda mwanamume na mwanamke wakahisi kwamba mataraja yao yametimia; lakini baada ya miaka fulani katika maisha ya ndoa, wanakata kauli kwamba hiyo ilikuwa ni ndoto tu! Maisha ya ndoa yasiposhabihi yale yanayosimuliwa katika riwaya za mahaba, wengi huona ndoa yao haiwezi kufaulu kabisa.
Pasipo shaka, matazamio fulani katika ndoa yanafaa kabisa. Kwa mfano, inafaa kutazamia upendo, ufikirio na utegemezo kutoka kwa mwenzi wa ndoa. Na bado, huenda hata matazamio hayo yasitimizwe. “Nahisi kana kwamba sijaolewa,” asema Meena, msichana mchanga aliyeolewa karibuni huko India. “Najihisi nikiwa mpweke na hakuna anayenijali.”
Kutopatana—“Hatupatani kwa Vyovyote”
“Hatupatani kwa vyovyote na mume wangu,” asema mwanamke mmoja. “Najuta kila siku kwamba niliolewa naye. Hatufaani kabisa.”
Kwa kawaida haichukui muda mrefu kwa wenzi wa ndoa kung’amua kwamba hawafaani kama walivyodhani wakati wa uchumba. “Maisha ya ndoa hufunua tabia zilizofichika wenzi hao walipokuwa waseja,” aandika Dakt. Nina S. Fields.
Kwa sababu hiyo, baada ya kufunga ndoa wenzi fulani wanaweza kukata kauli kwamba hawapatani kabisa. “Licha ya upatano fulani katika mapendezi na utu, watu wengi huingia katika maisha ya ndoa wakiwa na tofauti kubwa sana katika mtindo, tabia, na mielekeo,” asema Dakt. Aaron T. Beck. Wenzi wengi wa ndoa hawajui namna ya kutatua tofauti hizo.
Ugomvi—“Sisi Hugombana Daima”
“Tulishangazwa na ugomvi wetu wa kila mara—kurushiana maneno, na jambo baya zaidi, kunyamaziana kwa siku nyingi,” asema Cindy, akikumbuka siku za mapema za ndoa yao.
Kutokuelewana ni jambo la kawaida katika ndoa. Lakini hali hiyo ishughulikiweje? “Katika maisha mazuri ya ndoa,” aandika Dakt. Daniel Goleman, “mume na mke wako huru kulalamika. Lakini mara nyingi kwa sababu ya hasira, malalamiko hutolewa kwa njia yenye kuumiza na yenye kushambulia tabia ya yule mwenzi mwingine.”
Hali hiyo inapotukia, mazungumzo hugeuka kuwa mashindano, kila mmoja akishikilia maoni yake kwa ushupavu na hivyo hushambuliana kwa maneno badala ya kuwasiliana. Kikundi kimoja cha wataalamu chasema hivi: “Mojawapo ya matokeo mabaya zaidi ya ubishi usiodhibitiwa ni kwamba wenzi husema mambo yanayotisha usalama wa ndoa yao wenyewe.”
Ubaridi— “Tumeshindwa”
“Nimeshindwa kufanya ndoa yetu ifaulu,” akakiri mwanamke mmoja baada ya miaka mitano katika maisha ya ndoa. “Najua kwamba haitafaulu. Sasa nahangaikia watoto tu.”
Imesemwa kwamba kinyume kabisa cha upendo si chuki bali ni ubaridi. Kwa hakika, ubaridi waweza kuharibu kabisa ndoa sawa na uhasama.
Lakini jambo la kusikitisha ni kwamba, wenzi wengi wa ndoa wamevumilia ndoa isiyo na upendo kwa muda mrefu hivi kwamba hawana tumaini kabisa kwamba hali itabadilika. Kwa mfano, mume mmoja alisema kwamba maisha yake ya ndoa ya miaka 23 yalingana na “kufanya kazi isiyopendeza.” Aliongezea kusema: “Wajitahidi kufanya yale uwezayo katika hali hiyo.” Vivyo hivyo, mke aitwaye Wendy amekata tamaa kuhusu mume wake ambaye ameishi naye kwa miaka saba. “Nilijitahidi mara nyingi,” yeye asema, “lakini sikuzote alinitamausha. Niliishia kushuka-moyo. Sitaki kupatwa na hali hiyo tena. Nikimtumaini tena, nitajiletea tu uchungu. Afadhali nisitumainie chochote—sitakuwa na furaha lakini angalau sitashuka moyo.”
Kutamaushwa, kutopatana, ugomvi na ubaridi ni baadhi tu ya sababu zinazoweza kuchangia ukosefu wa upendo katika ndoa. Bila shaka, kuna sababu nyinginezo—sababu chache zinazungumziwa katika sanduku lililo kwenye ukurasa wa 5. Hata sababu iwe gani, je, kuna tumaini kwa wenzi ambao waonekana kuwa wamenaswa katika ndoa isiyo na upendo?

1 comment:

SIXBERTY MANSON POSTS

Mona Lisa

  MONALISA                              LA GIOCONDA                          By Sixberty Manson  A picture by Sixberty Manson  MEET THE REAL...

ZILIZOTAZAMWA ZAIDI